Vijiji 20 vya Ifakara, Kilosa kunufaika mpango wa mtumizi bora ardhi

Mkazi wa Kijijicha Kanolo, wilayani Ifakara Lucia Mbunda akionyesha mipaka ya shamba lake ili wataalamu wa ardhi wapime na kumpatia hatimiliki ya ardhi ya kimila.

Muktasari:

  • Ili kupambana na migogoro ya ardhi ikiwemo ya wakulima na wafugaji katika wilaya za Kilosa na Ifakara, Shirika la Kimataifa linalojihusisha na masuala ya ardhi la Landesa kwa kushirikiana na Shirika la Pelum Tanzania pamoja na Serikali wameandaa mpango wa matumizi bora ya ardhi kwenye vijiji 20.

Ifakara. Vijiji 20 vya Wilaya za Kilosa na Ifakara mkoani Morogoro vimeanza kufanyiwa mpango wa matumizi bora ya ardhi utakao kuwa tiba katika kupambana na migogoro ya ardhi ikiwemo baina ya wakulima na wafugaji.

Mbali na mpango huo wa matumizi bora ya ardhi, zaidi ya wananchi 16,000 wa vijiji hivyo watapimiwa vipande vya ardhi yao na kupewa hatimiliki za ardhi za kimila.

Mtaalamu wa Masuala ya Ardhi kutoka Shirika la Landesa Tanzania, Masalu Luhula amesema hayo jana Machi 21, 2022 katika kijiji cha Mang’ula, wilayani Ifakara wakati akizungumza kwenye mafunzo kwa vijana walioteuliwa kusaidia upimaji wa ardhi katika vijiji hivyo.

“Hadi mwezi Desemba mwaka huu tutakuwa tumekamilisha kazi ya upimaji wa ardhi na mpango wa matumizi bora ya ardhi kwa vijiji tisa,” alisema Masalu.

Alisema wamesamaliza kufanya mpango wa matumizi bora ya ardhi kwenye vijiji viwili vya Lumingo na Kanola na kwamba kazi inayoendelea sasa ni kupima ardhi ya wananchi kwa ajili ya kuwaandalia hatimiliki za ardhi za kimila.

Afisa Miradi wa Pelum Tanzania, Angolile Rayson mpango wa matumizi bora ya ardhi unasaidia katika kumaliza migogoro ya ardhi isiyo na tija kwenye jamii.

“Mpango wa matumizi bora ya ardhi unaishi kwa miaka 10 kwa hiyo kuna kuna vijiji vilifanyiwa mpango lakini umeisha, kwa hiyo tunahuisha na kuainisha maeneo muhimu ya kilimo, ufugaji, zahanati, mziko, shule na mengine,” alisema Angolile.

Ofisa Mpango Mji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa, Hillary Sandagila alisema kwenye wilaya yake, mradi huo utavifikia vijiji vitatu na kwa awali, wataanza kwenye kijiji cha Lumango ambacho wananchi hawajawahi kupewa hatimiliki za ardhi za kimila.

“Niseme tu wazi mpango huu wa matumizi bora ya ardhi ni msaada mkubwa kwetu kwa sababu tumetenga maeneo ya wakulima na malisho na tumekubaliana kila mtu akae kwake,” alisema.

Kwa upande wake, Afisa Mipango Miji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ifakara, Omary Tunduguru alisema kwenye eneo lake, vijiji tisa vinatarajiwa kunufaika kwenye mpango huo.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Kanolo, Said Ally amesema wananchi wake wapo tayari kupimiwa ardhi yao kwa sababu wanajua thamani yake.